Wafugaji wa nyuki na wauzaji wa asali wametakiwa kuepuka kuhifadhi asali katika chupa zilizotumika awali, zikiwemo chupa za maji au vinywaji baridi, ili kulinda ubora na thamani ya asali wanayozalisha.
Wito huo umetolewa na mtaalamu wa ufugaji nyuki, Johnson Ngondi january 30,2026 wakati akitoa elimu ya ufugaji nyuki wa kisasa kwa wafugaji katika kijiji cha Nkuu Sinde, Kata ya Machame Mashariki wilaya ya Hai.
Ngondi amesema kuhifadhi asali katika chupa zilizotumika husababisha asali kufyonza harufu iliyobaki kwenye vyombo hivyo, jambo linalochangia kupoteza ubora wake na kushusha thamani sokoni. Ameeleza kuwa wafugaji wanapaswa kutumia vyombo vipya maalum vya plastiki au chupa safi zenye muonekano wa kilichopo ndani, ambavyo havijatumika katika matumizi mengine.
Akizungumzia usalama wakati wa uvunaji wa asali, afisa nyuki msaidizi Halmashauri ya wilaya ya Hai Erick Cosma amesema matumizi ya vifaa maalum kama vazi la kinga na glovu humwezesha mfugaji kuwa salama zaidi na kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza wakati wa kuvuna asali.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Machame Mashariki, Jordan Ngowi, amesema mafunzo hayo yatasaidia wafugaji kuanza na kuendeleza ufugaji wa nyuki kwa kutumia mbinu za kisasa, hali itakayoongeza uzalishaji na kipato kwa wananchi wa eneo hilo.
Nao baadhi ya wanufaika wa mafunzo hayo, Wilson Shoo na Ana Masawa, wamesema elimu waliyoipata itawawezesha kufuga nyuki kwa tija zaidi, huku wakiwahamasisha wananchi wengine kuwekeza katika ufugaji nyuki wakisema ni shughuli yenye faida ya uhakika.
Kitongoji cha Bomani
Anuani ya Posta: 3 RD TTCL RC CHURCH 25382, P.O BOX 27 Hai
Simu: 0754553560
Simu ya Mkononi: 0754553560
Barua Pepe: ded@haidc.go.tz
Hatimiliki © 2017 Halmashauri ya Wilaya ya Hai